Mkuu wa mkoa wa Arusha Bwana Magesa Stanslaus Mulongo
ameelezea takwimu mbalimbali za mkoa wa Arusha katika mapambano dhidi ya
Ukimwi,dawa za kulevya na rushwa ambavyo ndivyo vinavyosisitizwa na ujumbe wa
mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka huu 2013.
Bwana Mulongo ametoa takwimu hizo wakati akipokea
mwenge huo kutoka mkoa wa Manyara katika kata ya kansai iliyopo kwenye mpaka wa
mikoa hiyo miwili ambapo mbio za mwenge sasa ziko rasmi katika mkoa wa arusha
ambapo miradi mbalimbali itazinduliwa.
Mkuu wa mkoa amemweleza Kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa
Bwana Juma Ali Simai kwamba;wananchi wa mkoa wake wameendelea kujitokeza kupima
ukimwi kwa hiyari mwaka hadi mwaka na kwamba,watu 122,442 wamepima ukimwi tangu
julai mwaka jana hadi sasa.
Amesema kati ya waliopima wanawake walikuwa 70,313 na
wanaume ni 52,129 ambapo jumla ya watu 1,834 walikuwa na virusi wanawake wakiwa
989 na wanaume 845 na kwamba kwa takwimu hizo kiwango cha maambukizi mapya
kimepungua kutoka asilimia 1.6 cha juni mwaka jana hadi asilimia 1.49 hivi
sasa.
Kuhusu biashara na matumizi ya dawa za kulevya Bwana Mulongo
amesema,biashara imekuwa kubwa na watumiaji wameongezeka ambapo hadi sasa jeshi
la polisi limeweza kukamata kila 77,581 za bangi,22,172 za mirungi na gramu 790
za kokein.
Aidha tangu julai mwaka jana hadi sasa jumla ya watuhumiwa
374 walihusika na makosa hayo na jumla ya kesi 140 zinazo husiana na dawa za
kulevya ziko mahakamani.
Kuhusu takwimu za rushwa,mkuu wa mkoa amesema;mkoa umepokea
taarifa 89 zinazohusiana na vitendo hivyo kuanzia mwaka jana hadi sasa na kesi
kumi ziko mahakamani.
Mwenge wa uhuru ukiwa mkoani Arusha utafanya kazi ya kuweka
mawe ya msingi,kuzindua na kufungua jumla ya miradi 54 yenye thamani ya
shilingi bilioni 5.9.
No comments:
Post a Comment